Waliosambaza taarifa kuhusu bei ya umeme nchini Tanzania kupanda, kukamatwa

"Nimeagiza hatua kali za kisheria zichukuliwe kwa kila aliyehusika na kueneza uongo kuwa TANESCO imepandisha bei ya umeme wakati wakijua fika sio kweli. Uenezaji wa taarifa za uongo...

0

Baada ya kutokea sintofahamu kwenye mitandao ya kijamii hapo jana kuhusu kupanda kwa gharama ya bei ya umeme, Waziri aliyepewa dhamana ya kusimamia Wizara ya Nishati, January Makamba, ametatua utata huo hivi leo Juni 9, bungeni jijini Dodoma.

Akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Nyasa kupitia tiketi ya CCM, Stella Manyanya aliyeuliza kuhusu uvumi huo kwenye mitandao ya kijamii, Makamba amekanusha uvumi huo kwa kusema kwamba, “Si kweli kwamba bei ya umeme imepanda, na Serikali inasikitishwa sana na kuvumishwa kwa taarifa hiyo ya uwongo”.

Makamba amesema kwamba, ameshaziomba mamlaka husika kuchukua hatua stahiki kwa wale wote wanaovumisha taarifa hiyo ya uzushi kuhusu kupanda kwa bei ya umeme nchini.

Pia, ametoa ufafanuzi ya kwamba, mchakato wa kupanda au kushuka kwa bei ya umeme si mchakato wa siku moja na wala haufanywi kwa siri, bali mchakato huu huusisha maombi ya TANESCO kwa EWURA na pia ni lazima Wananchi wahusishwe ili kutoa maoni yao ili mchakato ukamilike.

Hivyo basi, taarifa ya kwamba bei ya umeme imepanda, si ya kweli na ipuuzwe, amesema Waziri January Makamba.

Mara baada ya taarifa hiyo ya Makamba, Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Nnauye akaagiza hatua kali za kisheria zichukuliwe kwa kila aliyehusika kueneza taarifa hiyo

“Nimeagiza hatua kali za kisheria zichukuliwe kwa kila aliyehusika na kueneza uongo kuwa TANESCO imepandisha bei ya umeme wakati wakijua fika sio kweli. Uenezaji wa taarifa za uongo kiasi hiki ni uchochezi wenye lengo la kujenga chuki dhidi ya TANESCO na Serikali” Waziri Nape.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted