Rais mpya wa Sri Lanka, Ranil Wickremesinghe aapishwa

Waziri mkuu mara sita wa Sri Lanka Ranil Wickremesinghe aliapishwa Alhamisi kama rais wa Sri Lanka, akiwa na mipango ya kuunda serikali ya umoja ili kudhibiti machafuko hayo

0
Rais mteule Ranil Wickremesinghe akiapa kuwa Rais wa Sri Lanka katika bunge la Colombo. Waziri mkuu mara sita wa Sri Lanka Ranil Wickremesinghe aliapishwa kama rais mnamo Julai 21 “AFP PHOTO/Sri Lanka’s Parliament”

Waziri mkuu mara sita wa Sri Lanka Ranil Wickremesinghe aliapishwa Alhamisi kama rais wa Sri Lanka, akiwa na mipango ya kuunda serikali ya umoja ili kudhibiti machafuko hayo.

Mwanasiasa huyo mkongwe mwenye umri wa miaka 73, ambaye alichaguliwa kwa wingi wa kura kuwa mkuu wa nchi katika kura ya bunge Jumatano, alikula kiapo chake cha kuchukua wadhifa huo.

Duru rasmi za habari zilisema kiongozi huyo mpya anatarajiwa kuunda baraza la mawaziri hivi karibuni ili kuiondoa nchi hiyo katika mzozo mbaya zaidi wa kiuchumi tangu kupata uhuru kutoka kwa Uingereza.

Kiongozi wa upinzani Sajith Premadasa, ambaye alikuwa amemuunga mkono mgombeaji mpinzani wa urais katika kura ya Jumatano, alisema alikutana na Wickremesinghe kujadili jinsi ya kulinda nchi dhidi ya maafa zaidi.

“Sisi kama upinzani tutatoa msaada wetu wa kujenga nchi upya ili kupunguza mateso kwa rais wetu,” Premadasa alitweet Alhamisi.

Baraza la mawaziri la Wickremesinghe linatarajiwa kujumuisha wabunge kadhaa wa upinzani.

Mgogoro wa fedha za kigeni uliochochewa na janga la coronavirus na kuchochewa zaidi na usimamizi mbovu umeiacha Sri Lanka ikikabiliwa na kukatika kwa umeme kwa muda mrefu na mfumuko wa bei wa juu.

Watu milioni 22 nchini humo pia wamevumilia miezi kadhaa ya uhaba wa chakula, mafuta na dawa.

Hasira ya umma iliongezeka wakati makumi ya maelfu ya waandamanaji walipovamia nyumba ya rais wa wakati huo Gotabaya Rajapaksa, na kumlazimisha kung’atuka uongozini na kutoa nafasi kwa uchaguzi wa Wickremesinghe.

Wickremesinghe anatarajiwa sana kumteua rafikiye na waziri wa zamani wa utawala wa umma Dinesh Gunawardena kuwa waziri mkuu katika serikali ya umoja wa kitaifa.

Lakini vyanzo vya kisiasa vilisema kuwa wagombea wengine wawili pia walikuwa kwenye kinyang’anyiro hicho.

“Kutakuwa na wabunge wachache kutoka kwa upinzani mkuu watakaojiunga na baraza la mawaziri,” chanzo kilicho karibu na Wickremesinghe kilisema, na kuongeza kuwa alikuwa na nia ya kuhakikisha muungano wa vyama tofauti.

Wickremesinghe aliendesha bunge kwa saa 24 siku ya Alhamisi ili kuanza kikao kipya cha bunge, huku kinara mkuu wa serikali Prasanna Ranatunga akiwaambia wanahabari kuwa rais huyo mpya anataka kuunda upya kamati za bunge.

Utangazaji wa moja kwa moja wa hafla ya kuapishwa kwa Wickremesinghe katika jumba la bunge linalolindwa vikali ulikatizwa wakati yeye na mkewe Maithree walipoingia ndani ya jengo hilo baada ya kukagua gwaride la kijeshi.

Afisa wa ngazi ya juu wa ulinzi aliiambia AFP uchunguzi unaendelea ili kubaini kwa nini matangazo hayo yalikatizwa.

Kipaumbele cha serikali mpya ni kuendeleza mazungumzo ya uokozi wa kifedha kutoka kwa Shirika la Fedha la Kimataifa IMF na kulipa deni lake la nje.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted