Rais Samia,Ruto waagiza kuondolewa vikwazo 14 vya biashara

Rais Ruto amesema Mawaziri baina ya Kenya na Tanzania wanapaswa kufanyia kazi changamoto zilizobaki na kufikia mwishoni mwa mwaka huu changamoto zote zimetatuliwa.

0

Rais wa Kenya, William Ruto amesema mabishano yaliyokuwepo baina ya Tanzania na Kenya wameyaweka nyuma, lengo ni kuendelea kujenga uhusiano uliopo baina ya nchi hizo mbili.

Rais Ruto ameyasema hayo leo wakati akizungumza katika Ikulu ya Dar es Salaam akitaja baadhi ya mambo waliyokubaliana na Rais Samia Suluhu Hassan katika kuimarisha biashara na kukuza ushirikiano baina ya nchi hizo.

“Ile historia ya zamani kidogo mabishano tumeyaweka nyuma yetu, tunataka kujenga mahusiano mema, tunataka Watanzania wafaidike na tunataka Wakenya wafaidike, Wakenya wakifaidika na sisi, Tanzania itafaidika,”ameeleza.

Rais Ruto amesema wanataka kujenga uchumi wa pamoja na kukuza ushirikiano baina ya nchi hizo mbili na yapo mengi watayafanya wakiwa pamoja.

“Rais atahesabu ushirikiano wangu, Serikali yangu ipo tayari kufanya kazi kwa maslahi ya nchi zetu mbili,”amebainisha.

Pamoja na hayo Rais Ruto amebainisha kwamba Tanzania na Kenya wamekubaliana kuimarisha ushirikiano kudhibiti vitendo vya ugaidi na biashara haramu ya usafirishaji wa binadamu.

“Tumekubaliana vyombo vyetu vya ulinzi na usalama kushirikiana kuangalia makosa yanayovuka mipaka, madawa ya kulevya, uharamia, ujangili na usafirshaji wa watu,”amesema Rais Samia

Kwa upande wake Rais Samia amesema Tanzania na Kenya zinapata taswira mbaya ya usafirishaji wa binadamu.

Amesema kinachofanyika ni kuwakamata wahalifu pekee lakini kwenye rekodi za dunia taswira inakuwa mbaya, kuna haja kuchukuliwa hatua kudhibiti zaidi bishara hiyo.

Katika hatua nyingine Rais Samia Suluhu Hassan na Rais wa Kenya, William Ruto wametoa maagizo kwa mawaziri wa Uwekezaji kuhakikisha wanaondoa vikwazo 14 vya biashara baina ya nchi hizo.

“Kazi hii ilianza na Rais Mstaafu, Uhuru Kenyata na tulikubaliana kwa kuwataka wataalamu wetu kufanyia kazi vikwazo vya biashara vilipo.

“Mawaziri hao walitambua vikwazo 68 na vilifanyiwa kazi 54 na tumewataka sasa mawaziri wetu wakutane na kufanyia kazi vikwazo hivyo ili kuwe na uhuru wa kibiashara” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema ziara ya Ruto inatoa fursa ya kutathimini fursa ya ushirikiano katika ngazi zote

 “Tanzania na Kenya tusigawane umasikini na udhalili lakini tugawane utajiri tutakaofanya kupitia biashara,” amesema Rais Samia.

Kwa upande wake Rais wa Kenya, Willam Ruto amesema Serikali yake itaendelea kushirikiana na Tanzania akibainisha kwamba, kuondoshwa kwa changamoto hizo kumeinufaisha zaidi Tanzania ikilinganishwa na Kenya.

Amesema biashara baina ya Tanzania na Kenya imezidi kuimarika ambapo usafirishaji wa bidha kwa mwaka mmoja imepanda kutoka shilingi bilioni 27 kutoka Tanzania kufikia shilingi bilioni 50 kwenda Kenya.

Kwa upande wa Kenya amesema usafirishaji wa bidhaa kutoka Kenya kuja Tanzania imepanda kutoka shilingi bilioni 31 kufikia shilingi bilioni 45.

“Leo tunanunua vitu vingi kutoka Tanzania kuliko wanavyonunua kutoka Kenya na hii ni kutokana na ushirikiano baina ya nchi zetu.”ameeleza

Rais Ruto amesema Mawaziri baina ya Kenya na Tanzania wanapaswa kufanyia kazi changamoto zilizobaki na kufikia mwishoni mwa mwaka huu changamoto zote zimetatuliwa.

Rais Ruto yupo nchini Tanzania kwa ziara ya kikazi ya siku mbili ambapo aliwasili jana na leo amekutana na Rais Samia Suluhu Hassan na kufanya mazungumzo Ikulu, Dar es Salaam

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted