Inaumaa! Ghana yabanduliwa nje ya michuano ya AFCON

Mabingwa mara nne Ghana waliondolewa kwenye AFCON baada ya kuchapwa 3-2 na Wacomoro katika Kundi C Jumanne mjini Garoua.

0
Mashabiki wa Ghana katika mchuano wa AFCON uwanjani Stade Roumde Adjia mjini Garoua Januari 18 (Picha AFP)

Mabingwa mara nne Ghana waliondolewa kwenye Kombe la Mataifa ya Afrika baada ya kuchapwa 3-2 na Wacomoro katika Kundi C Jumanne mjini Garoua.

Nahodha wa The Black Stars Andre Ayew alitolewa kwa kadi nyekundu baada ya dakika 25. Walipoteza mechi hiyo baada ya Ahmed Mogni wa Comoro kufunga bao lake la pili dakika tano kabla ya mchezo kumalizika.

Morocco na Gabon zilitoka sare ya 2-2 mjini Yaounde katika kundi hilo hilo na kuhifadhi nafasi za kwanza na za pili mtawalia na kufuzu kwa awamu ya 16, itakayong’oa nanga Jumapili.

Comoro ni taifa dogo la visiwa kwenye ufuo wa kusini mashariki mwa Afrika, ilimaliza ya tatu na lazima isubiri hadi Alhamisi kufahamu ikiwa itakuwa miongoni mwa timu nne bora zilizo katika nafasi ya tatu, ambazo zitapata nafasi ya kuwa kati ya timu 16.

“Hatukuvunjika moya hata baada ya Ghana kusawazisha. Siku zote tuliamini tunaweza kuwa washindi,” alisema kocha wa Comoro Amir Abdou, ambaye amekuwa kocha tangu 2014.

“Tumeridhishwa na jinsi tulivyocheza. Tulikuwa na mpango na tulitimiza. Tulijifunza kutokana na makosa tuliyofanya katika michezo iliyopita. Ni wazi, sina furaha kwamba tulifungwa mara mbili, lakini tutaboresha.”

Mechi iliwaanzia vibaya Ghana baada ya dakika nne pekee pale El Fardou Ben Mohamed anayechezea Serbia alipofunga bao la kwanza na kuwaweka Comoro mbele.

Mogni, anayechezea klabu ya daraja la tatu ya Ufaransa, Annecy, aliongeza bao la pili baada ya saa moja tu na Ghana ikafunga mabao mawili kupitia wachezaji Richmond Boakye na Alexander Djiku.

Mogni alifunga bao la pili aliposukuma krosi ya chini chini kutoka kwa Ben Djaloud na kumpita kipa Joseph Wollacott na kuwapa Comoro ushindi.

Ghana ilikwenda Cameroon ikiwa na uhakika wa kufanya vyema baada ya kuishinda Afrika Kusini ili kujihakikishia nafasi ya kufuzu kwa Kombe la Dunia la 2022 nchini Qatar.

Timu ya Ghana ina kocha kutoka Serbia Milovan Rajevac na inajumuisha wachezaji watatu wa Premier League, beki wa Leicester City Daniel Amartey, kiungo wa Arsenal Thomas Partey na fowadi wa Crystal Palace Jordan Ayew.

Licha ya kupoteza kwa Morocco na kufungwa bao la dakika za lala salama dhidi ya Gabon, washabiki wa Black Stars walikuwa na uhakika wa kuifunga Comoro au hata kufuzu kuwa kati ya timu nne bora kwenye nafasi ya tatu.

Lakini hali ilizorota kwenye dakika 25 wakati Ayew, mwanawe gwiji wa Ghana Abedi “Pele” Ayew, alipoonyeshwa kadi nyekundu.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted