Tedros ateuliwa kama mgombea pekee kwenye uongozi wa WHO

Tedros Adhanom Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu WHO Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Afya Duniani Tedros Adhanom Ghebreyesus amehakikishiwa muhula wa pili baada ya kura ya kitaratibu Jumanne kumfanya kuwa...

0
Tedros Adhanom Ghebreyesus, Mkurugenzi Mkuu WHO

Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Afya Duniani Tedros Adhanom Ghebreyesus amehakikishiwa muhula wa pili baada ya kura ya kitaratibu Jumanne kumfanya kuwa mgombea pekee kabla ya uchaguzi wa viongozi mwezi Mei.

Kiongozi wa kwanza Mwafrika wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa alisema “anashukuru sana kwa uungwaji mkono upya,” baada ya bodi kuu ya WHO kupiga kura ya siri kuidhinisha kuteuliwa kwake kama mgombea pekee wa wadhifa huo.

Tedros, mmoja wa watu wanaotambulika zaidi katika vita dhidi ya UVIKO-19, alikiri kwamba muhula wake wa kwanza wa miaka mitano umekuwa wenye “changamoto na mgumu,” na akasema ni “heshima kubwa” kupewa fursa ya kuendelea na vita hivyo.

Waziri huyo wa zamani wa afya na mambo ya nje wa Ethiopia anatarajiwa kujitokeza kuchaguliwa tena wakati mataifa yote 194 wanachama wa WHO yatakapopiga kura kumchagua mkurugenzi mkuu mpya mwezi Mei.

Tangu UVIKO-19 ilipolipuka duniani zaidi ya miaka miwili iliyopita, mtaalamu huyo wa malaria mwenye umri wa miaka 56 amepokea sifa nyingi kwa jinsi alivyoiongoza WHO katika janga hilo.

Nchi za Kiafrika haswa zimefurahishwa na umakini unaotolewa kwa bara hili na kampeni yake kuhakikisha kuwa mataifa masikini yanapata chanjo ya UVIKO 19.

Ukosoaji kutoka Ethiopia

Chanzo kikuu cha upinzani dhidi ya kuchaguliwa kwa Tedros wakati huo huo kimetoka nchini mwake.

Serikali ya Ethiopia imekashifu matamshi yake kuhusu hali ya kibinadamu katika eneo alikozaliwa la Tigray, ambako mzozo ulidumu kwa miezi 14.

Baada ya Tedros kueleza kuhusu hai ilivyokuwa Tigray kuwa kama kuzimu na kuishutumu serikali kwa kuzuia dawa na misaada mingine muhimu kuwafikia walioathirika na mapigano hayo, Ethiopia ilidai achunguzwe kwa “utovu wa nidhamu na ukiukaji wa jukumu lake la kitaaluma na kisheria.”

Ethiopia, hata hivyo, haionekani kuwa na uungwaji mkono mkubwa katika kumkosoa Tedros.

Ethiopia iliizuia Umoja wa Afrika kuunga mkono kwa kauli moja uteuzi wa Tedros, lakini nchi kadhaa za Afrika, ikiwa ni pamoja na Kenya na Rwanda, na mataifa mengine 28  ya Ulaya yaliyowasilisha jina lake kuendelea na wadhfa huo

Amerika pia inamuunga mkono kwa kiasi kikubwa mkuu huyo wa WHO.

Kando na janga hilo, Tedros amekabiliwa na ukosoaji mkubwa, kutoka kwa mataifa yanayounga mkono muhula wake wa pili, juu ya kushughulikia kwake tuhuma mbaya za ubakaji na unyanyasaji wa kijinsia uliotekelezwa na wafanyikazi 21 wa WHO walipokuwa wakikabiliana na Ebola katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo kati mwaka 2018 na 2020.

Tedros aliiambia bodi kuwa “amesikitishwa” na ripoti hizo, akisisitiza WHO “haita vumilia kabisa unyanyasaji wa kingono.”

 Marekebisho muhimu

Muhula wa pili wa Tedros unaweza kutawaliwa zaidi na kazi kubwa ya kuimarisha WHO, udhaifu ambao umefichuliwa wakati janga hilo lilipoikumba dunia.

Nchi nyingi zinadai mageuzi makubwa, lakini kiwango cha mabadiliko bado hakijafafanuliwa, huku baadhi ya mataifa yanahofia kwamba WHO inaweza kuingilia uhuru wa mataifa yao.

Tedros pia anatoa wito wa mageuzi makubwa ya ufadhili wa WHO, akionya kuwa haina ufadhili unaohitajika kukabiliana na  mizozo mingi ambayo inawalazimu kukabiliana nayo duniani kote.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted