Takriban watu 80 wafariki kutokana na dhoruba Ana kusini mwa Afrika

Msumbiji na vituo vya hali ya hewa vya kimataifa vilionya kwamba dhoruba nyingine, iitwayo Batsirai, imezuka kwenye Bahari ya Hindi na inaelekea nchi kavu

0

Idadi ya watu waliofariki kutokana na dhoruba iliyopiga nchi tatu za kusini mwa Afrika imeongezeka hadi 77 siku ya Alhamisi wakati vikosi vya dharura vikipambana kukarabati miundombinu iliyoharibiwa na kusaidia makumi ya maelfu ya wahasiriwa.

Dhoruba Ana ilitua Jumatatu nchini Madagascar kabla ya kuelekea Msumbiji na Malawi ikileta mvua kubwa.

Wafanyakazi wa uokoaji katika nchi hizo tatu bado walikuwa wakitathmini kiwango kamili cha uharibifu, hata wakati dhoruba nyingine ilipokuwa ikitokea katika Bahari ya Hindi.

Alhamisi usiku Madagascar ilitangaza janga la kitaifa huku idadi ya waliofariki ikiongezeka hadi 48.

Dhoruba hiyo ilipita Zimbabwe, lakini hakuna vifo vilivyoripotiwa huko.

Katika nchi tatu zilizoathirika zaidi, maelfu ya nyumba ziliharibiwa. Baadhi ya nyumba zikiporomoka kutokana na mvua kubwa, na kuwafunika wengi  kwenye vifusi.

Mito iliyofurika ilisomba madaraja na mashamba, mifugo ilizama kwenye mafuriko hayo.

Huko Madagascar, watu 130,000 walikimbia makazi yao. Katika mji mkuu wa Antananarivo, shule na kumbi za michezo ziligeuzwa kuwa makazi ya dharura.

“Tulileta tu mali zetu muhimu zaidi,” Berthine Razafiarisoa, ambaye alipata makazi ya dharura kwenye jumba la mazoezi na familia yake ya watu 10, aliiambia AFP.

Kaskazini na kati mwa Msumbiji, Dhoruba Ana aliharibu nyumba 10,000 na makumi ya shule na hospitali, huku ikikata nyaya za umeme.

Msumbiji na vitu vya hali ya hewa vya kimataifa vilionya kwamba dhoruba nyingine, inayoitwa Batsirai, imezuka kwenye Bahari ya Hindi na inatarajiwa kufika nchi kavu katika siku zijazo.

Hadi vimbunga sita vya kitropiki vinatarajiwa kabla ya msimu wa mvua kuisha mwezi Machi.

Katika nchi jirani ya Malawi, serikali ilitangaza janga la kitaifa

Maeneo mengi ya nchi hayakuwa na umeme mapema wiki hii, baada ya mafuriko kufikia vituo vya uzalishaji umeme.

Umeme ulirejeshwa kufikia Alhamisi katika sehemu tofauti nchini.

Kusini mwa Afrika, na hasa Msumbiji, imekumbwa na dhoruba zenye uharibifu mara kwa mara katika miaka ya hivi karibuni.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted