Tume Ya Uchaguzi Na Mipaka Nchini Kenya (IEBC) Yaibua Vita Vya Kisiasa Kati Ya Rais Ruto Na Raila

Rais William Ruto ameteua jopo la wanachama saba ambalo litasimamia mchakato wa kuwachagua makamishana na mwenyekiti wa IEBC.

0
(Picha Hisani – Simon MAINA / AFP)


Tume ya Uchaguzi na Mipaka nchini Kenya (IEBC ) imeibua vita vipya kati ya Rais William Ruto na kiongozi wa upinzani Raila Odinga.

Februari 27,2023 Jopo ambalo lilitwikwa jukumu la kumchunguza kamishana wa (IEBC) Irene Masit ikiongozwa na jaji Aggrey Muchelule hatimaye iliwasilisha ripoti yake kwa Rais William,tume hiyo ikipendekeza Masit kuondolewa ofisini kwani alikwenda kinyume na maadili ya tume hiyo.

Masit ndiye kamishna pekee aliyekuwa amesalia katika tume hiyo ya uchaguzi nchini Kenya baada ya aliyekuwa mwenyekiti Wafula Chebukati na makamishna Boya Molu na Abdi Guliye kuondoka ofisini kufuatia kipindi chao cha kuhudumu cha miaka sita kufika tamati.

Baada ya kupokea ripoti kutoka kwa jopo la uchunguzi, rais William Ruto aliteua jopo lingine la wanachama saba ambalo litasimamia mchakato wa kuwachagua makamishana na mwenyekiti wa IEBC.

Jopo hilo linajumuisha Bethuel Sugut, Novince Euralia Atieno, Charity S. Kisotu, Evans Misati James, Benson Ngugi Njeri, Nelson Makanda na Fatuma Saman.

Hata hivyo mrengo wa upinzani umekuwa ukilalama kuhusu kutaka kuhusishwa katika mchakato wa makamishna wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini Kenya, IEBC.

Kulingana na kiongozi wa upinzani Raila Odinga, Rais Ruto kuhusika katika mchakato huu kutaathiri uwazi wa tume hiyo ya uchaguzi.

Raila alipendekeza majukumu ya kuwachagua makamishna wapya wa IEBC kupewa Jopo ambalo halitaegemea upande wowote, shinikizo ambalo alilijumuisha katika mojawapo ya makataa alimpa Rais Ruto ya siku 14 la sivyo waandae maandamano kote nchini.

Hata hivyo Rais William Ruto alimjibu Raila kwa kudai kuwa serikali yake halitakubali kutishwa na upinzani.

“Sote tupo sawa mbele ya sheria,na jaribio lolote ambalo litasababisha vurugu litakabiliwa na vitengo vya usalama ipasavyo. Serikali ya Kenya kwanza haitakubali vitisho. Mtaandamana tu kisha baadaye mtachoka,”alisema rais William Ruto.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted