Zelensky anasema ikiwa Ukraine itaanguka, mataifa mengine  ya Baltic pia yataanguka

Zelensky alitoa wito wa mazungumzo ya moja kwa moja na kiongozi wa Urusi Vladimir Putin, akisema "ndio njia pekee ya kukomesha vita hivi".

0
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky akizungumza na wanahabari mjini Kyiv Machi 3. – (Photo by Sergei SUPINSKY / AFP)

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky alitoa wito kwa nchi za Magharibi kuongeza msaada wa kijeshi kwa Ukraine, akisema Urusi inazidi kusonga mbele na kufikia maeneo mengine.

“Ikiwa huna uwezo wa kufunga anga, basi nipeni ndege!”

Zelensky aliuambia mkutano na waandishi wa habari.

“Ikiwa Ukraine itaangamizwa, Mungu atuepushie,basi nchi nyingine za Baltic za  Latvia, Lithuania, Estonia pia zitaanguka,” alisema na kuongeza: “Niamini”.

Alitoa wito wa mazungumzo ya moja kwa moja na kiongozi wa Urusi Vladimir Putin, akisema “ndio njia pekee ya kukomesha vita hivi”.

“Hatujaishambulia Urusi na hatuna mpango wa kuishambulia. Mnataka nini kutoka kwetu? Tuacheni ardhi yetu,”alisema akimwambia Putin.

“Keti pamoja nami. Sio umbali wa mita 30 tu kama (Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron),” kiongozi huyo wa Ukrain alisema, akimaanisha Putin kuwapokea viongozi wa dunia kwenye meza kwa mazungumzo.

Zelensky — ambaye wiki chache zilizopita alijaribu kuwatuliza Waukraine kuhusu madai ya Amerika kwamba Urusi ilikuwa inapanga kuivamia nchi yake — alisema: “Hakuna mtu aliyefikiri kwamba katika ulimwengu wa sasa mtu anaweza kufanya matendo ya kimnyama.”

Putin alizindua uvamizi wa Ukraine wiki iliyopita.

Urusi inasema hailengi maeneo ya kiraia licha ya kuwepo kwa ushahidi mkubwa kuwa wanalenga maeneo hayo.

Ukraine siku ya Jumatano ilisema ndege za Urusi ziligonga shule na kuua watu tisa katika mji wa kaskazini wa Chernihiv.

Kyiv inasema zaidi ya raia 350 wameuawa tangu Putin alipoanzisha uvamizi huo.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted