Martha Karua, Mgombea mwenza wa Raila Odinga

Martha Karua huenda akawa naibu rais wa kwanza mwanamke katika historia ya Kenya, iwapo Muungano wa, Azimio la Umoja One Kenya, utashinda uchaguzi wa Agosti 9.

0
Martha Karua, mgombea mwenza wa Raila Odinga

Mwanasiasa mkongwe na Waziri wa Sheria wa zamani Martha Karua huenda akawa naibu rais wa kwanza mwanamke katika historia ya Kenya, iwapo Muungano wa, Azimio la Umoja One Kenya, utashinda uchaguzi wa Agosti 9.

Siku ya Jumatatu tarehe 16 Mei, Martha Wangari Karua alitajwa kuwa mgombea mwenza wa Waziri Mkuu wa zamani Raila Odinga ambaye ndie kinara wa muungano wa Azimio One Kenya Party.

Karua anatoka eneo la Mlima Kenya na aliwahi kuwania kiti cha urais mwaka 2013 na kumaliza wa sita katika kinyang’anyiro hicho.

Uteuzi wake uliibua sherehe katika miji mikuu nchini Kenya, huku viongozi wa kike wakimsifu Raila kwa uamuzi wa kuchagua mwanamke kwa wadhfa huo wa mgombea mwenza.

Karua mwenye umri wa miaka 64 ni mwanasheria ambaye alihitimu kutoka Chuo Kikuu cha Nairobi mwaka wa 1980 na Shule ya Sheria ya Kenya mwaka wa 1981.

Alifanya kazi kama hakimu kabla ya kujiunga na siasa mwaka wa 1992, alipochaguliwa kuwa mbunge wa Gichugu, alihudumu kama mbunge wa Gichugu hadi mwaka wa 2013.

Kati ya 2003 na 2009, chini ya uongozi wa Rais wa zamani Mwai Kibaki – ambaye sasa ni marehemu – alihudumu kama waziri wa maji na baadaye kama waziri wa sheria.

Alijiuzulu kutoka wadhifa wa mwisho tarehe 6 Aprili 2009 akitaja kukatishwa tamaa katika kutekeleza majukumu yake.

Karua alikuwa miongoni mwa wale waliounda muungano wa kisiasa wa NARC ambao ulishinda Uchaguzi Mkuu wa 2002 na kuhitimisha uongozi wa KANU wa takriban miongo minne.

Baadae mwaka wa 2013 aliwania kiti cha urais kwa chama cha NARC Kenya bila mafanikio.

Katika uchaguzi wa mwaka wa 2017, aliwania kiti cha ugavana katika kaunti ya Kirinyaga tena bila mafanikio.

Martha Karua ni mama wa watoto wawili.

Mnamo 1991, Karua ilitambuliwa na Human Rights Watch kama mtetezi wa haki za binadamu

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted