Wagombea wanne wanaowania urais katika uchaguzi wa Kenya Agosti 9

Wagombea wanne wameidhinishwa kushiriki kinyang’anyiro cha kuwa rais wa Kenya, akiwemo naibu wa rais wa sasa William Ruto na Raila Odinga.

0

Wagombea wanne wameidhinishwa kushiriki kinyang’anyiro cha kuwa rais wa Kenya, akiwemo naibu wa rais wa sasa William Ruto na mwanasiasa Raila Odinga,Tume Huru ya Uchaguzi na mipaka IEBC ilisema.

Ndiyo idadi ndogo zaidi ya wagombeaji kupitishwa kugombea nafasi ya juu nchini humo tangu demokrasia ya vyama vingi mwanzoni mwa miaka ya 1990.

Ni wagombea wanne pekee ‘waliokidhi matakwa ya kikatiba na kisheria’ kutoka kwa orodha fupi ya 17, Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ilisema katika taarifa yake Jumatatu.

Kando na Ruto na Odinga, wagombea wengine wanaowania kiti cha urais katika kura ya Agosti 9 ni pamoja na mawakili David Mwaure na George Wajackoyah — jasusi wa zamani ambaye aliwahi kwenda uhamishoni Uingereza.

Zaidi ya wawaniaji 50 walikuwa wameonyesha nia ya kutaka kumrithi Rais Uhuru Kenyatta, ambaye lazima astaafu baada ya kuhudumu kwa mihula miwili ya miaka mitano.

Kinyang’anyiro cha mwaka huu kinaonkeana kuwa kati ya wagombeaji wawili kati ya mshirika wa zamani wa rais Ruto na kiongozi wa zamani wa upinzani Odinga mwenye umri wa miaka 77, ambaye sasa anaungwa mkono na Kenyatta.

Wajackoyah, ambaye ni mwanasheria, anawania kiti cha urais kwa ahadi ya kuongeza ofisi ya rais na kupunguza wiki ya kazi hadi siku nne na kuhalalisha bangi.

Mwaure, ambaye alionyesha nia ya kugombea mwaka wa 2013 lakini baadaye akaghairi kugombea, ameahidi kukabiliana na ufisadi ambalo ni suala gumu nchini Kenya.

Wagombea wenza wanawake

Wagombea wote isipokuwa Ruto wamechagua wanawake kama wagombea wenza wao, jambo ambalo, kama wangeshinda, litafungua milango kwa naibu rais wa kwanza mwanamke wa Kenya.

Akiwa mhimili mkuu wa siasa za Kenya, Odinga anasalia kuwa maarufu licha ya kufeli kushinda uchaguzi mara nne.

Ruto, 55, alipakwa mafuta na Kenyatta kama mrithi wake lakini akajikuta akitengwa baada ya mapatano ya 2018 kati ya rais na hasimu wake wa zamani Odinga.

Aliyekuwa waziri wa kilimo, Ruto amemkashifu Kenyatta kuhusu sera zake za kiuchumi ikiwa ni pamoja na mzigo mkubwa wa madeni nchini, akiahidi kutengua iwapo atachaguliwa.

Kwa kuwa Kenya ina jamii tofauti na makabila mengi, chaguzi nchini Kenya mara nyingi zimekumbwa na ghasia.

Kenyatta na Ruto walikuwa wamefunguliwa mashtaka na Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu kwa mashtaka ya uhalifu dhidi ya ubinadamu kwa madai ya kuhusika katika kuandaa ghasia za baada ya uchaguzi wa mwaka 2007 ambazo ziligharimu maisha ya zaidi ya 1,100.

Kesi hiyo ilisambaratika mwaka wa 2016 baada ya mahakama kutangaza kuwa imeshindwa ikitaja matukio ya kutatiza ya kuingiliwa na mashahidi.

Baada ya mapigano ya baada ya uchaguzi wa 2017 kusababisha vifo vya watu kadhaa, Kenyatta na Odinga walitangaza kujenga uhusiano bora wakisema wanatumai kumaliza mzunguko wa mara kwa mara wa ghasia zinazohusiana na uchaguzi.

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted