Macron awasili Cameroon katika mkondo wa kwanza wa ziara yake Afrika Magharibi

Macron anatazamiwa kufanya mazungumzo Jumanne asubuhi katika ikulu ya rais na mwenzake Paul Biya, 89, ambaye ametawala Cameroon kwa takriban miaka 40.

0
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron akitembea na Waziri Mkuu wa Cameroon Joseph Dion Ngute alipowasili kwenye uwanja wa ndege wa kimataifa wa Nsimalen Yaounde, Julai 25, 2022. (Photo by Ludovic MARIN / AFP)

Rais Emmanuel Macron aliwasili nchini Cameroon siku ya Jumatatu jioni akiwa mwanzoni mwa ziara ya mataifa matatu ya Afrika Magharibi huku akijaribu kujenga upya uhusiano wa Ufaransa baada ya ukoloni wake barani humo.

Macron alikaribishwa katika uwanja wa ndege wa Yaounde mwendo wa saa 10:40 jioni na Waziri Mkuu wa Cameroon Joseph Dion Ngute.

Safari ya kwanza ya muhula wake mpya nje ya Ulaya, ambayo pia itampeleka Benin na Guinea-Bissau, inalenga “kuonyesha dhamira ya rais katika mchakato wa kurejesha uhusiano na bara la Afrika,” alisema mwakilishi wa rais wa Ufaransa afisa ambaye aliomba kutotajwa jina.

Macron anatazamiwa kufanya mazungumzo Jumanne asubuhi katika ikulu ya rais na mwenzake Paul Biya, 89, ambaye ametawala Cameroon kwa takriban miaka 40.

Wanatarajiwa kujadili usalama nchini Cameroon, nchi ambayo imekumbwa na ghasia za kikabila na uasi wa watu wanaotaka kujitenga ambao wamekuwa wakipigania uhuru wa majimbo mawili yanayozungumza Kiingereza tangu 2017. Kaskazini mwa Cameroon pia imeshuhudia mashambulizi ya wanajihadi wa Boko Haram.

Macron alimkasirisha Biya mnamo 2020 baada ya kutangaza kuwa atatumia shinikizo kali kwa rais juu ya ghasia katika nchi hiyo ya Afrika Magharibi.

Ziara yake inakuja wakati ambapo Ufaransa iliyokuwa mamlaka ya kikoloni imeshuhudia ushawishi wake ukishuka ukitofautishwa na mataifa ya China, India na Ujerumani, hususan katika sekta za kiuchumi na kibiashara.

Baada ya chakula cha mchana na Biya na mkewe Chantal, Macron atakutana na wawakilishi wa vijana na mashirika ya kiraia.

Atamaliza siku katika ‘Noah Village’ iliyoandaliwa na bingwa wa zamani wa tenisi Yannick Noah, ambaye anaendeleza kituo cha burudani na elimu katika wilaya ya Yaounde, ambako anaishi kwa miezi kadhaa kwa mwaka.

Macron atakuenda Benin siku ya Jumatano, nchi ambayo imekabiliwa na mashambulizi mabaya kutoka kwa wanajihadi, ambao wameenea kutoka Sahel hadi mataifa ya Ghuba ya Guinea.

Benin ilisifiwa kwa muda mrefu kwa kustawi kwa demokrasia ya vyama vingi.

Lakini wakosoaji wanasema demokrasia yake imeporomoka kwa kasi chini ya Rais Patrice Talon katika kipindi cha nusu muongo uliopita.

Siku ya Alhamisi, Macron atakamilusha ziara yake nchini Guinea-Bissau, ambayo imekumbwa na mizozo ya kisiasa wakati ambapo rais wake, Umaro Sissoco Embalo, anajiandaa kuchukua usukani wa Jumuiya ya Kiuchumi ya Afrika Magharibi.

Nchi zote tatu zimeshutumiwa na wanaharakati kuhusu rekodi zao za haki, lakini Ikulu ya Elysee imesisitiza kuwa masuala ya utawala na haki yataibuliwa, ingawaje “bila muingilio wa vyombo vya habari lakini kwa njia ya mabadilishano ya moja kwa moja kati ya wakuu wa nchi.”

In this article

East Africa Premier News Source with Top Stories, Special Features and more.
Uncensored & Undaunted